Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.John Pombe Magufuli, ameendelea kukubalika kimataifa baada ya Jarida maarufu Duniani la Forbes kubashiri kwamba ataivusha Tanzania na kuwa nchi yenye kipato cha kati kupitia ajenda yake ya Tanzania ya viwanda chini ya mpango wa maendeleo wa 2025.

Katika jarida hilo la Forbes Afrika la Julai mwaka huu ambalo lilikuwa mahsusi kwaajili ya kelezea mafanikio ya Serikali ya Awamu ya Tano na uongozi wa Rais Magufuli kwa ujumla, imeelezwa maono yake kama kiongozi wan chi yameifanya Tanzania kupiga hatua kubwa za maendeleo na inatarajiwa kuwa miongoni mwa nchi chache sana za Afrika zenye maendeleo yanayoonekana na yanayopatikana kwa muda mfupi.

Kwamujibu wa Jarida hilo ambalo limemwelezea Rais Magufuli kama Tingatinga katika kusimamia kile anachokiamini, miongoni mwa mambo makubwa yanayomfanya ang’ae kimataifa ni pamoja na ujenzi wa reli ya kisasa ya standard Gauge SGR, upanuzi wa bandari na ujenzi wa miundombinu ya barabara zinazounganisha nchi nzima ambazo ni kichocheo kikubwa cha maendeleo hapa nchini.

Aidha Rais Magufuli ameelezewa kuwa ni mtu asiye na masihara katika kusimamia masuala ya maendeleo, mfano jinsi alivyosimamia na kuhakikisha uwanja wa ndege wa Julius Kambarage Nyerere terminal three unakamilika kwa wakati na kwa kiwango cha kimataifa.

Jarida la Forbes limeendelea kumwelezea Rais Magufuli kuwa, mafanikio mengi anayopata ni kutokana na kuongozwa na mpango wa maendeleo wa 2025 pamoja na ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya 2015.

Miradi mingine iliyoainishwa kuonyesha utendaji wake ni ile ya umeme ya Kinyerezi awamu ya kwanza ya pili nay a tatu, pamoja na mradi mkubwa wa kuzalisha umeme katika maporomoko yam to Rufiji maarufu kama Stieglers Gorge,ambayo lengo lake ni kumaliza kabisa tatizo la umeme hapa nchini hasa kwa wananchi wa vijijini.

Kuhusu ukuaji wa uchumi Jarida la Forbes limeelezea kuwa katika kipindi cha utawala wake tangu aingie madarakani mwaka 2015, uchumi umeendelea kukua kwa kasi kwa kiwango cha asilimia 7 ambao ni ukuaji wa mfano na wakuridhisha kwa nchi za Afrika ikilinganishwa na miaka mingi iliyopita.

Katika uwekezaji Rais Magufuli amenukuliwa akiwahakikishia wawekezaji na dunia kwa ujumla kwamba, Tanzania ni nchi salama na kwa uwekezaji na akawakaribisha kuja kuwekeza kwani ameendelea kufanya mapinduzi makubwa katika uwekezaji lengo kuu ikiwa ni kuvutia wawekezaji wengi zaidi.

Mahojiano ya Rais Magufuli yaliyotolewa na Jarida la Forbes Africa, yalifanyika mapema mwaka huu ambapo Jarida hilo lilikuwa na toleo maalum la Tanzania kuhusiana na mambo mbalimbali yanayotekelezwa na Serikali.

Credit: Michuzi