Waziri  wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, ameunda kamati ya watu wanne kuchunguza kifo cha Isululu Kabote (85), mkazi wa Kijiji cha Buhungukila, Wilaya ya Maswa mkoani Simiyu, ambaye anadaiwa kuuawa akiwa mikononi mwa polisi.

Kamati hiyo imeundwa baada ya wananchi wa kijiji hicho kudai kabla ya Kabote kukumbwa na mauti, Mei 17 saa 8:00 usiku, alikamatwa na askari polisi na kupigwa akidaiwa hajatoa mchango wa maendeleo wa Sh 50,000 madai ambayo Jeshi la Polisi limekanusha.

Naibu Waziri wa Madini, Stanslaus Nyongo ambaye pia ni Mbunge wa Maswa Mashariki (CCM), alisema kutokana na ukimya na polisi Mkoa wa Simiyu juu ya tukio hilo, aliiomba Serikali iundwe kamati hiyo ili kubaini ukweli wa tukio hilo.

Akiitambulisha kamati hiyo, Nyongo alisema kuna dalili za watu kulindana katika suala hilo kwa sababu tangu mzee huyo afariki, hakuna mtu aliyekamatwa.

“Kuna dalili za watu kulindana, wanafahamika waliosababisha kifo cha mzee wetu, lakini hatujasikia hata mtu mmoja ameshikiliwa na Jeshi la Polisi ili kusaidia uchunguzi, Polisi Mkoa wapo kimya, kwa kuundwa timu hii kila kitu kitajulikana,” alisema.

Alisema mwili wa marehemu umekaa siku 20 katika chumba cha kuhifadhia maiti kwa ajili ya uchunguzi wa kidaktari, taarifa ambayo itatumiwa na timu hiyo katika kubaini ukweli.

Nyongo alimtaja mwenyekiti wa timu hiyo ni Laifu Mella kutoka dawati la malalamiko Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi.

Wengine ni daktari bingwa wa mifupa kutoka Hospitali ya Rufaa ya Dodoma, Ibenze Ernest, Kefa Kaswamila kutoka Dawati la Malalamiko Kitengo cha Upelelezi Wizara ya Mambo ya Ndani na Mzee Mzee kutoka Ofisi ya Ofisa Usalama Mkoa wa Simiyu.