Afisa Mtendaji wa Kijiji cha Ibambilo Kata ya Bulega Wilayani Bukombe Mkoani Geita,Juma Maziku, amefariki dunia saa chache baada ya kuokotwa akiwa ametupwa kwenye barabara iendayo Mnekesi Wilayani Chato,huku mwili wake ukiwa na majeraha ya kushambiliwa na watu wasiojulikana.


Mkuu wa Wilaya ya Bukombe Said Nkumba akizungumza na Madiwani wa   Halmashauri ya Wilaya ya Bukombe Mkoani Geita amesema kitendo hicho hakikubaliki na kuahidi kuwasaka na kuwakamata wale wote waliohusika na tukio hilo.

"Kitu alichofanyiwa mtumishi huyu wa wananchi hakikubaliki kabisa, likemewe na kila mtu na kama kamati ya Ulinzi hatutafurahia inajurudia tena, tutahakikisha tunafanya msako ili watuhumiwa wachukuliwe hatua za kisheria." amesema DC Mkumba

Aidha,Mkuu huyo wa Wilaya amesema matukio kama hayo yanasababishwa na baadhi ya watumishi wa umma kuishi mbali na vituo vyao vya kazi na kuagiza ifikapo tarehe moja mwezi wa saba kila mtumishi awe amehamia na kuishi anakofanyia kazi.