Michuano ya Mataifa ya Afrika (AFCON) inatarajiwa kuanza Juni 21 nchini Misri huku timu zikiendelea na maandalizi. Tanzania inapeperusha Bendera kwenye michuano hii ikiwa kundi C ambalo lina timu nyingine ambazo ni Senegal, Kenya na Algeria, ambapo mchezo wa kwanza kwa Tanzania utakuwa Juni 23 dhidi ya Senegal.



Shirikisho la Soka Barani Afrika CAF limetoa zawadi za timu zitakazofanya vizuri katika kila hatua ya michuano hiyo, ambapo jumla ya dola 14.2 milioni zitagawanywa kwa timu nane bora, mgawanyo ambao utakuwa kama ifuatavyo.



Kwa upande wa timu itakayoibuka mshindi wa michuano hiyo, ataibuka na zawadi ya kitita cha dola milioni 4.5 sawa na shilingi bilioni 10 za Kitanzania.



Mshindi wa pili ataambulia dola milioni 2.5 sawa na shilingi bilioni 5.7, huku mshindi wa tatu akiambulia dola milioni 2.0 sawa na bilioni 4.6 za Kitanzania. Timu itakayotinga robo fainali inapewa dola 800,000 sawa na bilioni 1.8.



Kuelekea ufunguzi wa michuano hiyo, timu ya Wabunge 83 wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiongozwa na Spika, Job Ndugai inatarajia kuhudhuria ufunguzi wa mchezo wa Taifa Stars dhidi ya Senegal.