Na Leandra Gabriel, Blogu ya Jamii
TAASISI ya moyo ya Jakaya Kikwete imepokea wataalamu wa moyo kutoka Canada na Israel ambao watafanya upasuaji kwa  wa moyo kwa watoto 20 ndani ya wiki moja na hiyo ni kwa kushirikiana na madaktari bingwa wa moyo kutoka nchini.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete profesa Mohamed Janabi amesema kuwa taasisi ya Save a Chil's h Heart   kutoka Canada imekuja nchini zaidi ya mara tano kuanzia mwaka 2015 na ujio wao umekuwa na manufaa kwa kuwa walifundisha namna ya kufanya upasuaji kwa tundu dogo na safari hii wamewaalika wenzao kutoka nchini Israel nchi ambayo imetoa mafunzo kwa manesi wa uangalizi maalumu kutoka taasisi hiyo ya JKCI.

Janabi amesema ikiwa ni mara ya pili ya wataalamu hao kufanya upasuaji wa namna hiyo, wamelenga kuokoa maisha ya watoto huku akieleza kuwa upasuaji huo unatumia gharama nafuu na muda wa kulazwa ni mchache zaidi, (takribani siku 2 pekee.)

Amesema kuwa ushirikiano baina ya nchi hizo umekuwa na manufaa hasa katika kubadilishana ujuzi na kukutana kwa madaktari bingwa hao kwa muda wa wiki moja kutakuwa ni kwa kujifunza baina ya pande zote mbili.

Awali akieleza historia na majukumu yanayofanywa na taasisi hiyo Profesa Janabi amesema kuwa mikakati ya taasisi hiyo ni kuzidi kuwahudumia watoto wenye matatizo hayo kwa kushirikiana na wadau mbalimbali.

Amesema kuwa Serikali na wadau mbalimbali wamekuwa wakitoa ushirikiano katika kuhakikisha matibabu ya watoto hao yanafanikiwa na tayari mwezi uliopita manesi 2 wamepelekwa Nairobi, Kenya kwa ajili ya mafunzo hayo.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa taasisi ya Save a Child's Heart kutoka Canada Marni Brinder Byk amesema kuwa taasisi hiyo imedhamiria kuokoa maisha ya watoto pamoja na kudumidha mahusiano bora yenye tija kwa sasa na baadaye.

Brinder amesema kuwa wamefurahi sana kuja Tanzania na wanataraji kujifunza mengi kutoka taasisi hiyo pamoja na kudumisha mahusiano bora hapo mbeleni

Vilevile wakili na Mkurugenzi wa taasisi ya Save a Child's Heart kutoka Israel Simon Fisher amesema kuwa Tanzania ni nyumbani na wanaamini wataendelea kusaidia watoto Tanzania na kote duniani katika kuokoa maisha yao.
 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete Profesa Janabi Mohamedi akizungumza wakati kutambulisha ugeni wa madaktari bingwa kutoka Israel ambao watafanya upasuaji kwa watoto 20 ndani ya wiki moja, leo jijiji Dar es Salaam.
 Wakili na Mkurugenzi wa Taasisi ya Save a Child's  Heart kutoka Israel Simon Fisher akizungumza na waandishi wa habari ambapo amesema kuwa wamedhamiria kuokoa maisha ya watoto hao pamoja na kudumisha mahusiano bora ya sasa na baadaye, leo jijini Dar es Salaam.
 Baadhi ya wafanyakazi na madaktari wa Taasisi ya moyo ya Jakaya Kikwete.
Wataalamu na madaktari bingwa kutoka Israel na Canada (walioketi mstari wa mbele) wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Profesa Mohamed Janabi wakati wa kikao kazi kitakachowakutanisha madaktari hao katika kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto 20, leo jijini Dar es Salaam