Mwili wa kiongozi wa upinzani, Etienne Tshisekedi ambaye pia ni baba wa sasa wa rais wa DR Congo, Felix, unatarajiwa kuwasili nchini humo leo baada ya miaka miwili baada ya kifo chake. Kulingana na familia, mwili huo utawasili kutoka nchini Ubelgiji kwa mazishi.



Kwa mujibu wa BBC. Alifariki mjini Brussels akiwa na umri wa miaka 84 mnamo mwezi februari 2017 lakini mwili wake ulisalia katika mji huo wa Ubelgiji kutokana na wasiwasi wa kisiasa kwa utawala wa rais wa zamani wa taifa hilo Joseph Kabila.

Mazishi yake yatafanyika katika Viwanja vya Mashahidi, kulingana na nduguye Askofu Gerard Mulumba.

Mulumba anasema kuwa baada ya kuukaribisha mwili katika uwanja wa ndege , uatasafirishwa hadi katika uwanja huo kwa maombolezi .

Amesema kuwa tayari maandalizi katika uwanja huo ikiwezmo ujenzi wa jukwaa umekamilika mbali na yale ya maafisa wa polisi ambao wataongoza gwaride ili kumpatia heshima za mwisho baba huyo wa upinzani DRC.

Takriban marais watano wa bara la Afrika wamethibitisha kuhudhuria mazishi yake.

Mwanawe Tshisekedi felix Tshisekedi baada ya kuapishwa kuwa rais wa taifa hilo
Atazikwa kama shujaa.
”Ni zaidi ya miaka miwili tangu tulipoanza kutumia kila njia kuusafirisha mwili wake” , alisema Mulumba. ”Na sasa kwa kuwa hali iko shwari tunashukuru”, aliongezea.

Akiwa mwanasiasa wa muda mrefu, Tshisekedi alihudumu katika upinzani kwa miongo kadhaa lakini hakufanikiwa kuiongoza nchi hiyo.

Akiwa mkosoaji mkubwa wa aliyekuwa dikteta Mobutu Sese Seko, alianzisha chama cha Union for Democracy and Special Progress UDPS mwaka 1982 baada ya kuachiliwa kutoka jela.

Utawala wa Kabila
Joseph kabila
Mwaka 1997, baada ya Mobutu kung’atuliwa madarakani na kundi lililoongozwa naLaurent Kabila, Tshisekedi alianza kuwa mpinzani wa utawala mpya , msimamo aliokuwa nao hata baada ya mauaji ya Kabila 2001 huku mwanawe Joseph akipanda katika hatamu za uongozi.

Baada ya kushindwa katika uchuzi wa 2011 uliodaiwa kukumbwa na udanganyifu mkubwa , Tshisekedi alikataa kutambua utawala wa Kabila hadi kifo chake.

Miaka miwili baada ya kifo chake , mnamo mwezi Januari 24, mwanawe Felix Tshisekedi aliapishwa kuwa rais baada ya uchaguzi ambao ulimfanya Kabila kuondoka madarakani baada ya miaka 18.

Uchaguzi huo hatahivyo ulikumbwa na madai mengi ya udanganyifu huku siasa za taifa hilo bado zikitawaliwa na Kabila ambaye alijipatia umaarufu mkubwa akiwa madarakani.

Siku ya Jumatatu Tshisekedi alimteua mwanasiasa wa muda mrefu Sylvestre Ilunga Ilunkamba kuwa waziri mkuu.