Hammond Asema Brexit Bila Makubaliano ni Kitisho kwa Uingereza
Waziri wa fedha wa Uingereza Philip Hammond amewaonya watu wanaowania kurithi wadhifa wa waziri mkuu Theresa May kuachana na porojo ya kuondoka katika Umoja wa Ulaya bila makubaliano yoyote, na kuacha kutoa ahadi za matumizi ya bajeti yasiyotekelezeka.

 Akizungumza na shirika la utangazaji la Uingereza, BBC, Hammond amesema kuondoka kiholela kunaweza kuwa kitisho sio tu kwa uchumi wa Uingereza, bali pia kwa umoja wa taifa hilo. Mtu anayepewa nafasi kubwa ya kurithi mikoba ya Theresa May, waziri wa zamani wa mambo ya nje

Boris Johnson, amesema Uingereza itaondoka katika Umoja wa Ulaya ifikapo Oktoba 31, bila kujali kama makubaliano yamefikiwa na umoja huo au la. Philip Hammond pia amesema uchaguzi mpya hauwezi kumaliza mkwamo katika mchakato wa Uingereza kuondoka katika Umoja wa Ulaya, maarufu kama Brexit, kwa sababu vyama vikuu vya siasa vina mgawanyiko wa ndani kuhusu mchakato huo.