15 washikiliwa kwa kula pesa za vitambulisho
Katibu Tawala Wilaya ya Mbozi mkoani Songwe, Tusubilege Benjamin ameagiza jeshi la polisi kuwashikilia watendaji 15 wa vijiji na kata kwa tuhuma za kutafuna fedha zaidi ya milioni 15 za vitambulisho vya wajasiriamali.

Inaelezwa kuwa watendaji hao wamekula pesa za vitambulisho zaidi ya 762 vya wajasiliamali vilivyotolewa  na Raisi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli.

Akitoa agizo hilo, Katibu Tawala amesema kuwa kati ya watendaji 29 wa wilaya hiyo, ni watendaji 12 pekee wamesalimika kwenye mkasa huo huku mwenyekiti wa halmashauri hiyo, Ericki Minga akisisitiza hatua kali za kisheria kuchukuliwa kwa watendaji hao ambao wameitia doa halmashauri.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Halima Mpita amesema kuwa fedha za vitambulisho ni moja ya mapato ya nchi ambapo amewataka watendaji wa halmashauri kufanya kazi kwa weledi na uaminifu mkubwa .

Aidha Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi imegundua uwepo wa akaunti feki iliyokuwa inatumika kuiba fedha za halmashauri, huku Mkurugenzi ambaye uteuzi wake umetenguliwa wiki chache zilizopita, Kazimbaya Makwega Makwega akitajwa kuhusika na akauti hiyo feki iliyokutwa na kiasi cha sh milioni 83.