Vijana wa Chadema wanatua tena Dodoma ambako CCM inaendelea na maandalizi ya mwisho mwisho kwa ajili ya mkutano mkuu maalumu wa kumkabidhi Rais John Magufuli kiti cha uenyekiti.

Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema (Bavicha), Patrobas Katambi amesema wanatarajia kutua mjini humo kufanya mkutano wa kamati ya utendaji Julai 20 na Mwenyekiti wa chama chao, Freeman Mbowe atahudhuria.

“Polisi imepiga marufuku mikutano ya hadhara, siyo ya ndani. Sidhani kama kikao hiki watakizuia kwa sababu ni cha ndani,” amesema Katambi.
Amesema kikao hicho, kitajadili na kutoa mwelekeo wa masuala mbalimbali ikiwamo mkakati wao mpya wa kutafuta haki na demokrasia aliyodai inaminywa.