Siku 155 baada ya Dk John Magufuli kuapishwa kuwa Rais, aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema katika uchaguzi huo, Edward Lowassa ametaja mambo matano yanayomfanya autilie shaka mustakabali wa Taifa chini ya uongozi wa Rais huyo wa Awamu ya Tano. 


Akizungumza na wanazuoni wa ndani na nje ya nchi wakiongozwa na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (UDSM), Profesa Rwekaza Mukandala nyumbani kwake Masaki Dar es Salaam, Lowassa alisema: “Hali ya siasa nchini ni ya hamasa lakini isiyo na msingi endelevu.” 


Lowassa, ambaye alishika nafasi ya pili katika uchaguzi huo baada ya kupata kura milioni 6.07 sawa na asilimia 39.97 aliyataja mambo hayo kuwa ni Rais kugawa fedha wakati chombo cha kufanya hivyo kipo, watumishi kuachishwa kazi, upitishaji mizigo Bandari ya Dar es Salaam kushuka, nchi kunyimwa misaada na ugumu wa maisha unaowakabili wananchi hivi sasa. 


Katika uchaguzi huo, Rais Magufuli alipata kura milioni 8.8 sawa na asilimia 58.47 na kumshinda Lowassa ambaye alikuwa amejiunga Chadema Julai mwaka jana akitokea CCM ambako jina lake lilikatwa katika mchakato wa chama hicho kupata mgombea urais. 


Tangu aingie Ikulu, Rais Magufuli amekuwa akichukua hatua mbalimbali za kutengua uteuzi au kuwasimamisha kazi watendaji mbalimbali wa Serikali, kufuta maadhimisho ya sherehe mbalimbali na kuagiza fedha zitumike kutekeleza miradi mingine huku akiwabana wafanyabiashara kulipa kodi. 


Uamuzi wake huo unaofanywa pia na mawaziri wake umekuwa ukipongezwa na kukosolewa na watu wa kada mbalimbali na jana Lowassa alikuwa miongoni mwa wakosoaji hao ikiwa ni mara yake ya pili tangu Dk Magufuli aingie madarakani. 


Mara ya kwanza, Lowassa alikosoa sera ya elimu bure, alipoitofautisha na ile aliyokuwa ameahidi ya kuanzia awali hadi chuo kikuu na kuhoji iwapo Rais Magufuli mbali na ada angefuta pia michango mingine, jambo ambalo lilifanyiwa kazi. 


Alipoulizwa kuhusu mazungumzo hayo, Profesa Mukandala alisema: “Tunafanya utafiti kuhusu masuala mbalimbali ya kisiasa, uchumi, utawala bora na ushindani wa siasa na tunazungumza na watu kutoka vyama mbalimbali na viongozi wa Serikali.” 


Waziri wa Habari, Nape Nnauye alipoulizwa kuhusu kauli hiyo ya Lowassa alisema waziri mkuu huyo wa zamani anapingana na viongozi wa Chadema wanaokiri wazi kuwa Rais Magufuli anatekeleza sera na mikakati ya upinzani. 


Kauli ya Lowassa 
Taarifa iliyotolewa jana na ofisi ya Lowassa ilisema mwanasiasa huyo aliwaeleza wanazuoni hao kuwa; “hali ya siasa hivi sasa ni ya hamasa kutokana na Serikali mpya na ‘style’ mpya. Kwa kipindi kifupi atakuwa lakini hakuna mafanikio ya kiuchumi mbele ya safari.” 


Alisema Rais amekuwa akigawa fedha wakati chombo cha kufanya hivyo kipo ambacho ni Bunge. 


Rais Magufuli amekuwa na utaratibu kuidhinisha fedha zilizotengwa kwa ajili ya sherehe mbalimbali kutumika katika shu ghuli nyingine. Juzi, aliagiza Sh2 bilioni zilizokuwa zitumike katika Siku ya Muungano zitumike kupanua barabara inayokwenda Uwanja wa Ndege wa Mwanza. 


Pia, amewahi kuamuru Sh4 bilioni za Siku ya Uhuru kupanua Barabara ya Morocco – Mwenge, Dar es Salaam. 


Aliagiza pia fedha za maadhimisho ya siku ya Ukimwi kutumika kununua vifaatiba na Sh225 milioni zilizotengwa kwa ajili ya hafla ya uzinduzi wa Bunge zilinunulia vitanda Hospitali ya Taifa Muhimbili. 


Lowassa pia alieleza kusononeshwa na hali ngumu ya maisha na idadi kubwa ya watu kuachishwa kazi. 


“Nasononeshwa ninapoona watu wanaachishwa kazi na mashirika mbalimbali kwa sababu ya hali ngumu ya uendeshaji wa mashirika hayo. 


“Bandarini sasa hivi nasikia uingizaji mizigo umeshuka kwa asilimia 50, kampuni nyingi za mizigo zimefunga shughuli zake na pale kulikuwa na vijana wetu wengi wana ajira, sasa hivi wako mitaani, hali inatisha maisha ya mwananchi yanazidi kuwa magumu,” alisema. 


Lowassa aligusia uamuzi wa Marekani kupitia bodi yake ya Changamoto za Milenia (MCC) kusitisha msaada wa zaidi ya Sh1 trilioni. 


“Ni pigo kwa mustakabali wa uchumi. Halafu tunasema tunataka nchi ya viwanda, hela tutatoa wapi kama si hawa wafadhili wa ndani na nje kusaidia katika hilo?” alihoji. 


Lowassa ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema alisema: “Hawa wafadhili siyo watu wa kuwabeza wataturudisha nyuma. Jakaya (Kikwete- Rais mstaafu wa Awamu ya Nne) kwa kiasi kidogo alijitahidi kuvutia wawekezaji, japo kulikuwa na uzembe na ufisadi katika kuwasimamia. 


“Hapa kinachotakiwa ni kufanya mabadiliko katika mfumo na kuufanya kuwa endelevu,” alisema. 


Alisema si kweli kuwa kila mtu katika Serikali ya Awamu ya Nne alikuwa mla rushwa huku akikiri kuwa mfumo wa Serikali hiyo ulikuwa mbovu na wa kifisadi. 


Aliwaeleza wanazuoni hao kuwa: “Uchaguzi ule tulishinda (upinzani) na kila mtu anajua hivyo. Hata Magufuli anajua hilo...,” alisema. 


Akizungumzia mikakati ya upinzani, Lowassa alisema wamejipanga kuhakikisha hawaporwi tena ushindi na kusisitiza kuwa joto la kutaka mabadiliko bado ni kubwa na Watanzania wameichoka CCM. 


Kauli na Nape 
Akijibu hoja zilizotolewa na Lowassa, Nape alisema, “Anajichanganya tu, maana Mbowe (Freeman – Mwenyekiti wa Chadema) amenukuliwa akisema Rais Magufuli anaiga kila kitu cha Chadema, sasa yeye (Lowassa) anaposema hayo maana yake haelewani na Mbowe.” 


Alisema litakuwa jambo la ajabu kama Lowassa atakubali kila jambo linalofanywa na Serikali iliyopo madarakani kwa kuwa ndivyo alivyo. 


“Katika Uchaguzi Mkuu Lowassa hakuchaguliwa na wananchi ila Magufuli alichaguliwa kwa sababu wananchi walifurahishwa na sera zake, hivyo amuache mwenzake atekeleze ahadi zake kwa wananchi,” alisema Nape. 


“Kwanza Lowassa amekuwa mtetezi wa wezi, mafisadi na wala rushwa. Unawateteaje watu wa aina hii wanapofukuzwa kazi. Amebanwa tu na kwake kazi inayofanywa na Magufuli inampa maumivu.”